Powered By Blogger

Jumatatu, Mei 08, 2017

Momogoro blog: wabunge wastushwa na kukubali kukatwa posho

WABUNGE wameelezea kushtushwa na msiba wa watoto 33 uliotokea Arusha huku wakitaka kukatwa posho zao kwa ajili ya rambirambi kwa wazazi wa watoto hao. Sambamba na hilo, wameshauri wanafunzi waliopona kwenye gari hiyo wapatiwe tiba ya akili kwa kupewa ushauri nasaha ili wasiathirike kisaikolojia.
Akizungumza na gazeti hili, Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya (Chadema), ameshauri leo Bunge liahirishwe ili kuungana na Watanzania kuomboleza msiba huo wa kitaifa na kufafanua “mbona tunaahirisha Bunge kwa kifo cha mtu mmoja hivyo hawa ni wengi tuahirishe pia.” Aliwashauri wabunge wenzake kukubali kukatwa posho za siku mbili kwa ajili ya kutoa rambirambi kwa wazazi wa watoto hao.
Kwa siku mbunge analipwa Sh 220,000 kama posho ya kikao. “Nilivyosikia taarifa hizi nilipandwa na shinikizo la damu nikashindwa kwenda kwenye mechi kati ya wabunge na Benki ya NMB na nilikuwa mchezaji. Mimi pia ni mama na nina mtoto wa darasa la sita, tuwaombee wazazi wa watoto hao kwani msiba ni mzito sana,” aliongeza Bulaya. Naye Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema), ambaye anatokea mkoani Arusha, alitaka Bunge na Taifa kuonesha limeguswa na msiba huo ulitokea kwa shule iliyoongoza kimkoa na kiwilaya mwaka jana kwa kikao cha Bunge leo kusitishwa.
Alitaka serikali kuonesha imeguswa na msiba kwa kushiriki kikamilifu na kuongeza “iliwahi kutokea Arusha watu chini ya ishirini walipoteza maisha kwenye machimbo ya mchanga kwa kuangukiwa na kifusi, aliyekuwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alikuja msibani, serikali iliwapa fedha wafiwa na ilinunua majeneza.” Mbunge wa Mkinga, Dustan Kitandula (CCM), alisema ni msiba wa kitaifa kwani taifa limeondokewa na nguvu kazi iliyotegemewa kuja kuhudumia taifa. Alishauri kufanyike utafiti nchi nzima wa maeneo maarufu kwa ajali za mara kwa mara ili hatua zichukuliwe na kuokoa maisha ya watu.
“Mtoto aliyebaki kwenye ajali nashauri ahamishwe shule ingawa hilo ni utashi wa mzazi na wengine wote walio kwenye gari nyingine ambao wamepona wafanyiwe tiba ya akili, wapewe ushauri nasaha kwani tukiacha wataathirika hata kwa miaka ya baadaye,” alishauri Kitandula. Mbunge wa Mbinga, Sixtus Mapunda (CCM), mbali na kusikitishwa na kuwataka wazazi wapewe moyo, alisema kwa mazingira ya ajali husika, wote waliokuwapo kwenye basi lile hawakufunga mkanda na hiyo imechangia wengi kupoteza maisha.
“Wangefunga mkanda kwenye ile coaster lazima wengi wasingekufa hasa waliokaa nyuma maana unaona kabisa kule kulikuwa salama, pia madereva sasa wadhibitiwe kudhibiti mwendo,” alieleza Mapunda. Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Ester Mmasi (CCM), aliwataka wamiliki wa shule kuwekeza zaidi kwenye usalama wa wanafunzi kama inavyotumia nguvu nyingi kuwekeza kwenye biashara ya shule kwa kufunga vidhibiti mwendo, ili uongozi wa shule ujue gari linapokwenda na kasi inayokuwa nayo na si kumtegemea dereva kumlinda mtoto. “Ukiangalia ile ajali unaona kabisa gari lilikuwa chakavu, nina shaka na uimara wake, nashauri wenye shule watumie magari yaliyokaguliwa na Sumatra na ubora uangaliwe na TBS,” alieleza Mmasi.

Toa maoni yako Kupitia Facebook.com/proffesa%nazirhamzatz

MOMOGORO BLOG:Wazazi wasimulia jinsi walivyo uona huo msiba mkubwa.

TAIFA liko katika maombolezo makubwa ya msiba wa wanafunzi 33, walimu wawili na dereva wa Shule ya Msingi ya Mchepuo wa Kiingereza ya St Lucky Vincent, ambao walikufa baada ya gari lao kutumbukia kwenye korongo la Mto Marera, Kata ya Rhotia wilayani Karatu mkoani Arusha juzi asubuhi huku baadhi ya wazazi wakisimulia jinsi waliovyoupokea msiba huu mzito.
Tangu baada ya taarifa za ajali za msiba huo kusambaa katika mitandao ya kijamii, siku nzima ya juzi ikawa ya majonzi makubwa ambayo yameendelea kwa siku nyingine ya jana na zaidi leo wakati itakapofanyika ibada maalumu kwenye Uwanja wa Michezo wa Shehe Amri Abeid Kaluta, katikati ya Jiji la Arusha. Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, alitarajiwa kutua jana jijini humo na leo anatarajiwa kuongoza mamia ya wakazi wa Arusha na mikoa ya jirani watakaohudhuria ibada maalumu itakayofanyika uwanjani hapo kwa ajili ya heshima ya watu hao 36 waliopoteza maisha wakiwa safarini kwenda katika mitihani ya ujirani mwema mjini Karatu.
Mbali ya Makamu wa Rais, viongozi wengine wa serikali watakaoshiriki ibada hiyo ni Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana.
GAMBO ATOA RATIBA Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo aliwaambia wanahabari jana kuwa viongozi hao wamethibitisha kushiriki ibada hiyo itakayoanza saa mbili asubuhi. Gambo alisema miili yote ya wanafunzi waliokufa katika ajali hiyo itakuwepo kwenye uwanja huo na kufanyiwa ibada kabla ya kuchukuliwa na ndugu, jamaa kwa ajili ya kwenda katika maziko mahali watakapokuwa wamekuchagua.
Aliwataka Watanzania waliopo jijini Arusha na nje ya Arusha kuja kwa wingi katika ibada hiyo yenye simanzi kubwa kwa Watanzania wote kote nchini. Wanafunzi hao walipata ajali katika eneo la Rhotia na gari aina ya Mitsubishi Rosa lenye namba za usajili T871BYS lililokuwa likitoka jijini Arusha kwenda katika Mji wa Karatu kupata ajali ya kutumbukia mtoni na kusababisha vifo hivyo. Wanafunzi hao waliondoka jijini Arusha saa mbili asubuhi kuwahi mtihani huo wa majaribio wa kirafiki na wenzao wa Shule ya Msingi ya Tumaini Junior ya Karatu.
MAJINA YA WALIOKUFA Majina ya wanafunzi walikufa wametajwa kuwa ni Aisha Said, Anold Alex, Gladness Goodluck, Junior Mwashuy, Praise Ronald, Witness Moses na Heavenlight Mcharo. Wengine ni Eliapenda Eliudi, Rukia Halfan, Justine Alex, Rehema Msuya, Irene Kishari, Prisca Charles, Ian Tarimo, Shedrak Bikhet, Sabrina Saidi, Rachel Gidion, Irene Moses, Hagai Lucas.
Pia wamo Rehema Eliwadi, Rebeca Daudi, Dismas Kessy, Innocent Papian (mwalimu), Oumuh Rashid, Gema Gerald, Grayson Masawe, Julius Bonge Mollel (mwalimu), Joel Lucas, Naomi Hosea, Ruth Ndemno, Saada Ally, Neema Martin, Witness Philemon na Musa Khamis. Aidha, kwa mujibu wa mtu wa mtumishi wa chumba cha maiti Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru, ambaye hakupenda kutaja jina lake, baadhi ya miili ya watoto hao imehamishiwa Hospitali ya Selian kwa sababu mochwari ya Mount Meru ilikuwa imejaa, hivyo maiti zilizohamishiwa huko ni saba ambazo ni Neema Martin, Oumuh Rashid, Gema Mchome, Irene Moses, Rebeka Daudi, Hagai Lucas na Rachel Gidion.
Wazazi na walezi walikusanyika tangu asubuhi ya jana kwenye Hospitali ya Mount Meru kwa ajili ya kuwaona watoto hao huku wakisoma majina yaliyobandikwa ili kujua kama wapo hospitali hiyo au Hospitali ya Selian. WAZAZI WASIMULIA WALIVYOPOKEA MSIBA Katika hatua nyingine, badhi ya wazazi wameelezea jinsi walivyopokea msiba kwa huzuni na wengine wakisema ni jambo la kushukuru kwa yote kwani mapenzi ya Mungu yametimizwa.
Wakizungumza katika maeneo tofauti ya Kwamrombo katika eneo la Baa Mpya na Mtaa wa Mlimani Kata ya Terrat, baadhi ya wazazi hao walioondokewa na watoto wao, walisema inaumiza kwani baadhi ya watoto walikuwa wakikaa shuleni wakiwa darasa la saba huku wengine wakitokea nyumbani kwenda ziara ya kimasomo Karatu. Mzazi wa marehemu Irene Moses (13) ambaye ni Mosses Kivuyo anayefanya kazi Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga ambaye sasa yupo masomoni Chuo cha Ufundi Arusha, alisema mtoto wake Irene alikwenda Karatu na wenzake, lakini ghafla alisikia taarifa kuwa watoto hao wamepata ajali.
Alisema hakujua kama mwanawe ni miongoni mwa waliokufa, lakini alijipa moyo na kisha kuanza safari ya kutoka Arusha kwenda Rothia kwa ajili ya kuona watoto hao akiwemo mwanawe Irene na alipokuwa njiani, alipigiwa simu na wauguzi wakisema mtoto wake anataka kufanyiwa upasuaji, lakini wameamua kwanza wampigie simu. ASHUHUDIA MWANAWE AKIKATA ROHO Alisema aliwajibu wauguzi hao kwamba yuko njiani anakwenda na alipokaribia eneo la tukio hakumwona binti yake hivyo akaenda hospitali sababu alipigiwa simu kwani mtoto wake ndiye alisema apigiwe simu akiwa majeruhi “ndipo niliondoka kwenda kumuona Hospitali ya Karatu kumuona ndipo nilipofika tu mtoto wangu namuona akifa.” “Ukweli nimeumia kama mzazi.
Huyu ni mtoto wangu wa kwanza kati ya watoto watatu sasa huu msiba ni mzito sana kwetu wazazi tulioondokewa na watoto... inauma jamani, lakini haya ni mapenzi ya Mungu nashukuru kwa hili. Lakini nimeumia nafika tu hospitali mtoto anakufa jamani Irene wangu,” alieleza Moses. Naye mzazi wa marehemu Oulu Rashid, Msagaya Kimea alisema taarifa za mtoto wake kufa alizipata kupitia mitandao ya kijamii akiwa nyumbani kwake Kwamrombo, alipomuona mkewe akilia.
Alimwacha nyumbani kisha yeye kutoka hadi barabarani kupiga simu kwa Meneja wa Shule ya Lucky Vicent ili kuthibitisha taarifa hizo na meneja huyo alimweleza juu ya tukio hilo kisha alikwenda Hospitali ya Mount Meru kwa ajili ya kuona miili ya watoto hao. AONA JINA KUPITIA MITANDAO Alisema alikaa hospitali kwa muda mrefu kusubiri watoto wao waletwe, lakini ghafla aliona kupitia mitandao ya kijamii majina ya watoto waliokufa likiwamo jina la mwanawe.
“Nilishtuka nikajipa moyo maana sikujua kama mwanangu huo ndio ulikuwa mwisho wake maana alihamia shuleni kukaa huko, yaani nimeumia lakini ni jambo la kushukuru Mungu kwa kila jambo “. Awali shuleni hapo wakizungumzia tukio hilo, Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Lucky Vicent, Severine Laswai, alisema ajali hiyo ni huzuni kubwa kwa wananchi, walimu ndugu, jamaa na marafiki na jumla ya wanafunzi waliopata ajali hiyo ni 33 wakiume wakiwa ni 13 na wakike 20, walimu wawili na dereva mmoja Alisisitiza kuwa huu msiba ni wa kitaifa hivyo hawezi kuongelea zaidi juu ya tukio hilo kwani hivi sasa wanaandaa taarifa zaidi, lakini alisisitiza kuwa hilo ni pigo kubwa kwao.
DEREVA WA SHULE Naye Mkuu wa Shule hiyo, Ephraim Jackson, alisema nipo katika wakati ngumu sana. “Kwa kweli siwezi kuongelea suala hili kwa undani sana, lakini nataka kuwaambia kuwa dereva aliyekufa ni dereva wa shule yangu ni mwajiriwa hapa shuleni na hilo gari ni gari la shuleni kwangu wala sijakodisha,” alibainisha. “Yanasemwa mengi, lakini huyu dereva ambaye ni marehemu ni dereva wangu na hilo gari lililopata ajali ni gari la shule.
Huu ni msiba mzito na unaniumiza sana,” alisema Jackson. Kwa mujibu wa wafanyakazi shuleni hapo, wanadai kuwa dereva huyo ana mwaka mmoja kazini na alikuwa akiendesha gari dogo la shule na hiyo ilikuwa ni safari yake ya kwanza kwenda mbali na kuendesha basi kubwa. Aidha, baada ya ajali hiyo, wanafunzi wengine waliokuwa katika mabasi mawili kati ya matatu yaliyokuwa katika msafara huo, walirejea shuleni kwa kutumia mabasi yao ya shule kisha kuruhiswa kurejea nyumbani na wazazi wao waliokuwepo shuleni hapo.
LA SABA WALIKUWA 106 Alisema watoto walikwenda kwenye ziara ya kimasomo na ni utaratibu wa shule kwenda kushindana na shule zingine huku akisema shule hiyo ya Lucky Vicent English Medium ilianza mwaka 2006, na wanafunzi wanaotarajia kumaliza darasa la saba wakiwa ni 106, lakini sasa watabaki 73 baada ya wenzao hao 33 kufariki juzi. “Siwezi kusema zaidi ya haya kwa kweli maana nimeumia juu ya watoto hawa maana tumewafundisha wengine tangu shule za awali na hadi sasa wamekuwa wakubwa ndiyo wanakufa.
Ukweli sisi tumepata pigo kama walimu watoto hawa tumewazoea na leo hii wamekufa kweli kama walimu tumepata ganzi kwenye miili yetu, sijui tutafundishaje maana hii picha haitatutoka mapema,” alisema Jackson. Kwa upande wake, mwalimu Julius huku akilia alisema, “Hii ni huzuni fikiria watoto mnawafundisha leo hii unaona kabisa mwanga wa maisha yao wengine wakiniona walikuwa wakisema mwalimu nataka kuwa daktari, mwingine nesi, na wengine walitamka kazi zao, leo hii ndoto zao zimezimika ghafla, kweli huu msiba ni mgumu.
“Siwezi kusema moyoni juu ya tukio hili jinsi nilivyoumia, lakini najiuliza watoto wengine wakirudi shuleni kuendelea na masomo hali itakuwaje, marafiki zao hapa shuleni je watasemaje, tutawajibu nini watoto hawa yani naanza kuandaa majibu ya kujibu watoto hawa ambao ni wadadisi wa mambo.” MEYA: KILA MTAA UNALIA Awali Meya wa Jiji la Arusha, Calist Lazaro, alisema msiba huo ni mzito kwani kila mtaa watu wanalia. Naye Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, akitoa pole shuleni hapo, alisema amehuzunika juu ya msiba huo kwani umezima ndoto za watoto hao katika kupata elimu na kusisitiza kuwa huo ni msiba mbaya na kuna mambo ya kujifunza juu ya msiba huo ikiwemo masuala ya kurekebisha, hivyo mengine atayaongela bungeni.
“Poleni sana wazazi, walezi, ndugu jamaa na marafiki wote waliokumbwa na msiba huu mzito, kuna mambo mengi ya kujifunza katika msiba huu, lakini nawapa pole wote maana huu msiba ni mbaya sana,” alieleza Lema. SERIKALI KUGHARIMIA SANDA, MAJENEZA Serikali itagharamia sanda na majeneza kwa ajili ya wanafunzi waliopoteza maisha mapema juzi kwenye ajali iliyokuwa ikihusisha safari ya kimasomo.
Akitoa taarifa hiyo jana, Meya wa Jiji la Arusha, Calist Lazaro, alisema taarifa za awali zinaonesha kuwa tayari serikali imekwishalipia gharama za majeneza na sanda ya kuhifadhia miili ya marehemu ambao leo wanatarajiwa kufanyiwa ibada kwenye Uwanja wa Shehe Amri Abeid Kaluta. Lazaro alisema viongozi mbalimbali wakiwemo mawaziri pamoja na wabunge walikusanyika katika eneo la shule jana kwa ajili ya vikao vya kuandaa ibada hiyo.

Toa maoni yako Kupitia Facebook.com/proffesa%nazirhamzatz

Jumapili, Mei 07, 2017

Yanga yatimua vumbi kweli

YANGA jana ilirudi kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Bara baada ya kuifunga Prisons mabao 2-0 katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam. Matokeo hayo yanaifanya Yanga kufikisha pointi 59 sawa na Simba, lakini ikiongoza kwa uwiano mzuri wa mabao.
Simba leo inatarajia kucheza na African Lyon kwenye uwanja huohuo wa Taifa, mechi inayotabiriwa kuwa ngumu kwa upande wake. Iliilazimu Yanga kusubiri hadi kipindi cha pili kuandika bao hilo baada ya Prisons kuonekana kujipanga vizuri kwa kipindi chote cha kwanza.
Amisi Tambwe aliwainua vitini mashabiki wa Yanga waliofika uwanjani hapo baada ya kufunga bao la kuongoza katika dakika ya 71 akiunganisha mpira wa krosi iliyochongwa na Juma Abdul.
Dakika tano baadaye Obrey Chirwa aliwaandikia mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu bao la pili akiunganisha vema pasi ya Geofrey Mwashiuya. Bao hilo lilizidi kuwachanganya Prisons ambao sasa walionekana kurudi nyuma wote kuzuia mabao zaidi baada ya Yanga kuonekana kufunguka zaidi kushambulia.
Kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Toto African imejisogeza mpaka nafasi ya 13 kwenye msimamo wa ligi hiyo huku ikiishusha JKT Ruvu baada ya kuifunga mabao 2-1. Ruvu sasa inasubiri kumaliza ratiba na kuungana na timu nyingine mbili zitakazofanya jumla ya timu tatu zitakazoshuka daraja kwani sasa hata ikishinda mechi zote zilizosalia haiwezi kupanda.
Katika mechi ya jana, Ruvu ilikuwa ya kwanza kuandika bao la uongozi katika dakika ya kwanza likifungwa kwa shuti kali na Hassan Dilunga ndani ya 18. Toto ilichomoa bao hilo dakika ya 20 kupitia wa Waziri Junior akiunganisha krosi ya Mohamed Soud kabla ya kuunganisha mpira kwa kichwa na kuujaza wavuni.
Junior aliifungia tena Toto bao la pili katika dakika ya 35 akiunganisha pasi ya Jamal Soud. Katika mechi nyingine zilizochezwa jana, Majimaji imeendelea na harakati zake za kupambana kubaki Ligi Kuu baada ya kuifunga Mwadui mabao 3-0 kwenye uwanja wa Majimaji Songea, Ruvu Shooting ikiwa nyumbani Mabatini Mlandizi ililazimishwa sare ya bao 1-1 na Kagera Sugar

Toa maoni yako
Kupitia Facebook.com/proffesa nazir Hamzatz

UKUMBI WA MAHABA (chukua tafadhari juu ya mambo haya kabla ya kujiingiza kwenye mahusiano)

HAKUNA ubishi kuwa kila mwanadamu katika dunia hii, anahitaji kupendwa na kuwa katika uhusiano wa kimapenzi. Kutokana na ukweli huo, wengi wetu tumekuwa tukipata tabu inapofikia hatua ya kuingia katika uhusiano, kwani huwa na matarajio makubwa na wenza wetu kiasi cha kujikuta tunaishia kuwa na uhusiano wa kila aina, yote hiyo ni katika kutafuta wenza angalau wanafikia matarajio yetu.
Enzi za mababu zetu, masuala kama hayo, yalikuwa hayana haja, kwani kulikuwa na utamaduni wa watu kuchaguliwa wenza wao wa maisha ambao baadaye hujikuta wakipendana na kuanzisha familia kutokana na mazoea.
Hata hivyo, hali kwa sasa ni tofauti sana na zamani, kwani wengi wetu hujichagulia wenza wetu wa kuwa na uhusiano nao ikiwa ni pamoja na kuanzisha nao familia. Hivyo basi, ili kuepuka lindi la kuvunjika kwa uhusiano ambao katika miaka ya sasa hali hiyo imekuwa ni kawaida, ni vyema kwanza kabla ya kuingia kwenye uhusiano ukajihadhari na mambo yafuato.
Epuka kujiingiza kwenye uhusiano kama bado hauko tayari. Wapo watu wanajikuta wanapata tabu ya kuendelea kudumisha uhusiano walionao kutokana na kujiingiza kwenye uhusiano walipo wakiwa hawako tayari kuwa kwenye uhusiano.
Unakuta mtu mwingine ametoka kwenye uhusiano mbaya au hata hajajiandaa wala kujiwekea malengo ya kuwa na uhusiano wa namna gani au vitu anavyovitaka kwa mwenza wake, lakini anajikuta anapapukia kwenye uhusiano tu ghafla matokeo yake uhusiano husika huvunjika kutokana na wawili hao kutofautiana.
Na katika eneo hilo, pia jiepushe na mwenza asiye na malengo ya maisha au kuwa na uhusiano wa kudumu. Tukiri tu kuwa wapo wanawake na wanaume wanaotaka kuwa kwenye uhusiano wa muda mfupi kwa maana ya kwamba hawana mpango wa kuwa na uhusiano wa kudumu na kuwa na familia.
Watu wa aina hiyo, ni hatari sana kuanzisha nao uhusiano kwani pindi wanapotimiza malengo yao, bila kujali hisia zako watakuacha wewe ukiendelea na maumivu ya moyo. Japokuwa hili si lazima sana, lakini ni vyema kabla hujaingia kwenye uhusiano, uhakikishe angalau mwenza utakayekuwa naye uwe na vitu kadhaa mnavyoendana tofauti na hapo uhusiano huo utakuwa na wakati mgumu.
Ni kweli kuwa watu wanaweza kuvumiliana na kuishi pamoja hata kama wana tabia tofauti, ila kama tofauti ni kubwa sana, kuna hatari ya kuburuzana na kama hakuna mvumilivu uhusiano huo unaweza kuwa njia panda.
Hizi sifa zilizotajwa hapo juu sio za kina sana, lakini ni mojawapo ya mambo ya kuzingatia katika kuchagua mwenza wako wa maisha kabla ya kujizamisha katika mapenzi. Je wewe unaona ni mambo gani ya kuzingatia katika mahusiano na ni mambo gani yanasababisha ndoa kuvunjika? \ Usisite kuandika maoni yako kupitia
Facebook.com /proffesa nazir Hamzatz

Kampuni zaalikwa maonesho ya madini

KAMPUNI ya wazawa ya Sky Associated Group ya Arusha inayomiliki mgodi wa TanzaniteOne ni miongoni mwa kampuni pekee iliyojitokeza kuuza madini aina ya tanzanite kwenye Maonesho ya Sita ya Madini.
Mnada huo unafanyika kwa siku tatu katika maonesho hayo kwa kushirikiana na Shirika la Madini la Taifa (Stamico) ambapo mara baada ya ukamilishwaji wa uuzaji wa madini hayo, serikali itapata mapato.
Hayo yalisemwa jana na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Madini katika Wizara ya Nishati na Madini, Profesa James Mdoe wakati alipozungumza kuhusu uuzaji wa madini hayo kwa mnada kwenye maonesho hayo yaliyoanza jana hadi Mei 5, mwaka huu.
Profesa Mdoe alisema kampuni hiyo ni pekee iliyojitokeza kuuza madini yake katika mnada huo unaofanyika kwenye maonesho hayo, lakini pia wachimbaji wadogo nao wamesisitizwa kutumia fursa hiyo kuyatangaza madini hayo pamoja na kuyauza kwa wafanyabiashara wakubwa wanaohudhuria maonesho hayo kutoka nchi mbalimbali.
“Tulitoa muda kwa kampuni nyingine za madini ya tanzanite kushiriki katika maonesho haya, lakini hazijajitokeza, hivyo Kampuni ya TanzaniteOne ndio itakayouza madini haya katika maonesho haya na natoa rai kwa wachimbaji wadogo kuongeza umahiri zaidi katika kuweka nakshi pamoja na kupata masoko ya ndani na nje ya nchi,” alisema.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dk Joel Bandera ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maonesho hayo ya vito, alisisitiza kuwa ni vyema sasa serikali ikajenga jengo la Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje (EPZ) wilayani Simanjiro ili kuwezesha madini hayo kuuzwa kwa wingi na wageni kutoka nchi mbalimbali kuja kuwekeza nchini.
Dk Bendera alisema madini hayo hayapatikani maeneo mengine, bali Tanzania pekee hivyo ni vyema yakaongezwa thamani ikiwemo kupatikana kwa soko la uhakika ili kila mwananchi ayanunue badala ya wageni kutoka nchi nyingine kuyanunua na kuvaa kama vito.
Awali, akitembelea maonesho hayo, mmoja kati ya washiriki, Osman Abdulsattar kutoka Kampuni ya Gem Tanzanite Ltd, alitoa rai kwa serikali kuondoa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye madini ya tanzanite ili Watanzania wanunue na kuvaa kama vito na wengine kutumia kama mapambo kwenye miili yao

DC(mkuu wa wilaya ya Ilala kula sahani moja na wanaokwamisha kodi

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema, amesema hatawafumbia macho wenyeviti wa Serikali za Mitaa watakaokuwa kikwazo cha wananchi kulipa kodi za majengo kwa kuwa jambo hilo si la kisiasa.
Aidha, Wenyeviti wa serikali za mitaa katika wilaya hiyo wamekubali mamlaka ya ukusanyaji wa kodi za majengo kukabidhiwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuwa itasaidia katika kukusanya kiwango sahihi.
Akizungumza wakati wa kufungua semina ya siku moja kwa wenyeviti wa serikali za mitaa, Watendaji wa Kata na mitaa, Mkuu huyo wa wilaya alisema, suala la ukusanyaji wa kodi si jambo la kisiasa bali ni kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wote.
“Sitegemei nyinyi mkawe kikwazo cha wananchi kulipa kodi, nategemea hatatokea mmoja wenu akasimame na kuwa kikwazo. Hatutakubali mtu asimame kati ili kukwamisha wananchi wasilipe kodi, huyo tutamchukulia hatua na katika hili sitataka mchezo,” alisema Mjema.
Akizungumzia semina hiyo, Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Manispaa ya Ilala, Ubaya Chuma, alisema wanaamini hatua hiyo kwa sasa itasaidia kwa kuwa yapo mambo ambayo yamerekebishwa.
Kwa upande wake, Naibu Kamishna wa Kodi za Ndani, Yusuf Salum Yusuf, alisisitiza kuwa kwa sasa fedha zitakazokuwa zikikusanywa zitaerejeshwa kwa wakati ili mitaa iweze kufanya maendeleo yake.
Alisema kwa mwaka 2015/16 walikuwa na lengo la kukusanya Sh bilioni 7.82 lakini kwa mwaka huu wa fedha 2016/17 lengo lao ni kukusanya Sh bilioni 12.5, ambayo ni ongezeko la asilimia 55.

Ajali mbaya iliyotokea Arusha Jana Asubuhi , baadhi ya wanafunzi wakiingizwa hospitalini

MASHUHUDA waliofika kwanza kwenye eneo la tukio la ajali mbaya iliyotokea jana asubuhi walikuta wanafunzi 37 na walimu waliokufa kwenye ajali hiyo wakiwa wamelundikana sehemu ya mbele ya basi hilo lililokuwa limeharibika vibaya.
Kukiwa hakuna muathirika hata mmoja katika viti, wengi wanaamini kuwa watoto waliokuwa wameingiwa hofu walitoka kwenye viti vyao na kukimbilia kwa walimu wao baada ya gari kuanza kuyumba.
Mkazi wa Rhotia, Nancy Baha alisema aliona basi hilo la shule likiwa katika mwendo kasi lakini katika mtindo wa kuyumbayumba, ikiwa ni asubuhi yenye ukungu kabla yeye na mashuhuda wengine waliokuwa dukani kushuhudia kwa macho yao basi hilo lenye rangi ya njano likirushwa juu na kudumbukia korongoni, likitanguliza sehemu ya mbele.
Watu wengine walioshuhudia ajali hiyo wanakumbuka watoto wakipiga kelele, ni dhahiri watoto hawa kabla ya kupatwa mauti walishuhudia jambo la kutisha maishani mwao. Inadaiwa kuwa lori lililokuwa likija mbele ndio lilisababisha dereva wa basi kutoka nje ya barabara kwa lengo la kukwepa kugongana uso kwa uso na ndipo basi lilitumbukia kwenye korongo la Mto Marera.
Mistari mitatu ya viti vya nyuma vya basi hilo aina ya ‘Mitsubishi Rosa,’ lenye namba za usajili T-871 BYS, vilikutwa kama vilivyo, hivyo waliofika mapema eneo la tukio kwa ajili ya kuokoa majeruhi wanaamini wanafunzi kwa woga walitoka kwenye siti zao na huenda walikuwa wanakimbilia kwa walimu wao waliokuwa wamekaa mbele kwa ajili ya msaada au huenda walikuwa wanajaribu kukimbilia mlango.
Wakati taifa likiwa katika msiba huu mzito, kutokana na vifo vya wanafunzi wa darasa la saba zaidi ya 35 na walimu wao watatu, watu waliofika wa kwanza eneo la ajali walisema miili yote ilikutwa eneo la mbele la basi hilo.
Wanafunzi hao na walimu wao waliondoka Arusha saa 2.00 asubuhi, pengine dereva alikuwa katika haraka kufika wanakokwenda kuwahi muda wa mtihani katika shule ya Tumaini English Medium iliyopo wilayani Karatu.
Ajali imetokea karibu saa 4:00 asubuhi.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alithibitisha idadi ya watu waliokufa kuwa ni wasichana 16, wavulana 17 na watu wazima wanne akiwemo dereva, hata hivyo mtoto wa 38 inadaiwa amekufa baadaye katika Hospitali ya Mount Meru. Watoto wanne na mtu mzima mmoja wamenusurika kifo lakini wamejeruhiwa.
Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Esther Mahawe alitembelea majeruhi katika Hospitali ya Wilaya ya Karatu kuwajulia hali. Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Theresia Mahongo, alisema wanafunzi wa shule ya Lucky Vincent walikuwa njiani kwenda mji wa Karatu kushiriki mtihani wa moko wa kirafiki na wenzao wa Shule ya Msingi ya Tumaini Junior, Karatu. Basi hilo ni mali ya shule ya Lucky Vincent likiwa na Bima ya Zanzibar.
Mmiliki wa shule Innocent Mushi hakupatikana kwa sababu siku nzima simu yake ilikuwa imezimwa. Mushi ni mfanyabiashara anayemiliki shule ya Lucky Vincent na biashara ya usafirishaji mkoani humo.
Jambo la ajabu, wiki iliyopita, moja ya gari la Mushi aina ya Scania liligonga mwanafunzi wa shule nyingine katika eneo la Sakina. Katika eneo la shule Kwa-Mrombo, wazazi, ndugu na marafiki waliokuwa wamejaa huzuni kubwa walikuwa wamekusanyika na hali hiyo ilikuwepo pia katika kambi ya polisi Arusha kwani baadhi ya watoto waliokufa ni wa maofisa wa polisi.
Majina ya marehemu
Majina ya marehemu yaliyotajwa hadi sasa kutokana na ajali hiyo ni Mteage Amos, Justine Alex, Irene Kishari, Praise Ronald, Shadrack Biketh, Junior Mwashuya, Aisha Saidi, Heri Rashid, Gema Gerald, Rebecca Daudi, Hagai Lucas, Sada Ally, Lucy Ndemna, Mussa Kasim na Neema Martin. Wengine ni Witness Mosses, Rukia Khalfani, Naomi Hosea, Hevenight Hosea, Eliapenda Eliudi, Arnold Alex, Marion Mrema, Rehema Msuya, Sabrina Said, Prisca Charles, Grayson Robson Massawe, Lara Tarimo na Neema Eliwahi.
Wote walikuwa wanafunzi wa darasa la saba ambao walikuwa wafanye Mtihani wa Taifa wa Shule Msingi 2017 . Shule hiyo pia iliongoza mitihani ya taifa mwaka jana. Shule ya Awali na Msingi ya Lucky Vincent ambayo wanafunzi wake wameteketea katika ajali hiyo jana asubuhi waliongoza mwaka jana katika Mtihani wa Taifa Kimkoa.
Shule hiyo iliyopo eneo la Field Force, Kwa-Mrombo katika kata ya Olasiti, mjini Arusha ilikuwa shule ya 20 bora kati ya shule 8,109 nchini na katika Mtihani wa Taifa wa Darasa la Saba mwaka jana ilikuwa na wahitimu 101 na wanafunzi wote waliofanya mtihani walipata Daraja A katika somo la Kiingereza.
Shule ya Msingi Lucky Vincent ilikuwa shule namba moja mkoani Arusha na kuzishinda shule nyingine za msingi 331 katika wilaya saba za mkoa huo. Wakati wanafunzi wote wa Lucky Vincent walipata ‘A’ kiingereza, wanafunzi 92 walipata ‘A’ kwenye somo la sayansi , 81 walipata ‘A’ ya hesabu na 63 walipata ‘A’ Kiswahili (63), ikionesha walikuwa wazuri katika masomo ambayo wengine wanayaona magumu sana.
Katika hatua nyingine, Mwalimu Mkuu Msaidizi, Longino Vincent alisema amehuzunika sababu jana asubuhi yeye ndiye aliyepanga orodha ya wanafunzi hao na kwa sababu walipanda magari matatu kila gari walipanda wanafunzi 32 na walimu wao na kulielezea tukio limemfanya apate mshituko mkubwa baada ya kusikia ajali hiyo.
Kwa mujibu wa Vincent, chanzo cha ajali hiyo ni kuwa gari lilikosa breki ndipo dereva alipohangaika nayo na kutumbukia kwenye korongo hilo lililosababisha wanafunzi na walimu wao kupoteza maisha.
Alisema watoto hao waliondoka saa 12:30 asubuhi na safari yao ilikuwa ya saa mbili tu kutoka Arusha hadi Karatu jumla ya watoto hao walikuwa 96 na walimu wao. “Gari lilikosa breki dereva wetu Denis alikuwa akihangaika kujaribu kuokoa maisha ya watoto wetu lakini haikuwezekana ndipo likatumbukia kwenye korongo,… hili gari limepata hitilafu na kwa sababu dereva alikuwa katikati ndipo aliamua aingie hapo kwenye korongo akidhani ni dogo kumbe ni korongo kubwa na walimu wawili waliokufa ni Innocent Papian ambaye ni Mwalimu wa kingereza na Julius Mollel Mwalimu wa sayansi,” alisema.
Mkuu wa wilaya ya Arusha, Gabriel Fabian Daqqaro alisema ibada ya kuwaombea watoto waliokufa katika ajali itafanyika kesho saa tatu asubuhi katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid na taratibu za mazishi kufanywa.
Rais John Magufuli atuma rambirambi
Katika hatua nyingine, Rais John Magufuli amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya vifo vya wanafunzi wa darasa la saba, walimu na dereva wa gari la shule ya msingi iitwayo Lucky Vincent ya Arusha vilivyotokea jana saa tatu asubuhi baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali katika eneo Rhotia Marera, Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu ilisema kwa masikitiko Rais Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo na kueleza kuwa ajali hiyo imezima ndoto za watoto waliokuwa wakijiandaa kulitumikia Taifa na imesababisha uchungu, huzuni na simanzi kubwa kwa familia za marehemu na Taifa kwa ujumla.
“Ndugu Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo naomba unifikishie pole nyingi kwa wazazi, ndugu, jamaa na marafiki wote wa wanafunzi, walimu na dereva waliopoteza maisha, hiki ni kipindi kigumu kwetu sote, na uwaambie naungana nao katika majonzi na maombi,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Rais aliongeza kusema kuwa, “muhimu kwa sasa tuwaombee marehemu wote wapumzishwe mahali pema, majeruhi wapone haraka na wote walioguswa na msiba huu wawe na moyo wa subira, ustahimilivu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.”
Spika wa Bunge atuma salamu za pole
Wakati huo huo, Spika wa Bunge Job Ndugai amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo kutokana na vifo vya wanafunzi, walimu na dereva wa Shule ya Msingi Lucky Vicent ya mkoani Arusha, baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali jana asubuhi katika eneo la Rhotia Marera, wilayani Karatu, mkoani Arusha.
“ Mkuu wa Mkoa nakupa pole sana, nimepokea kwa mshtuko taarifa hii ya ajali iliyogharimu maisha ya watoto wetu, hakika hili ni pigo kwa taifa zima, namuomba Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi,” alisema Ndugai.
Aliongeza kuwa, “natoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki waliopoteza wapendwa wao, Mwenyezi Mungu awape nguvu na faraja katika kipindi hiki kigumu, vilevile nawaombea majeruhi wote wa ajali hiyo wapate uponyaji wa haraka.”
Katika hatua nyingine, Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe, amesema chama chake kimepokea kwa majonzi na simanzi kubwa taarifa ya vifo vya wanafunzi pamoja na waalimu wao.
Taarifa kwa vyombo vya habari ilisema Zitto alisema taifa limepoteza nguvu kazi ambayo si rahisi pengo lake kuzibwa na kuwapa pole waalimu wa shule ya awali na Msingi ya Lucky Vicent, wazazi wa watoto, ndugu, jamaa na marafiki ambao wamepoteza vipenzi vyao.
Kiongozi huyo wa ACT aliomba kwa Mwenyezi Mungu majeruhi wapone haraka na waweze kuendelea na masomo yao mpaka wafikie malengo waliyotarajiwa. “ACT- Wazalendo tumesikitishwa na vifo hivi vya watoto wetu pamoja na walimu wao, tunawapa pole ndugu jamaa na marafiki Mwenyezi Mungu awape nguvu ya kuhimili kipindi hiki kigumu kwao… Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi, Amini,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Wakati huo huo, wakati tunakwenda mtamboni wazazi walikuwa wakitambua miili katika hospitali ya Mount Meru. Tukio hili la wanafunzi wa Lucy Vincent, linakumbusha tukio lingine baya ambalo taifa lilipata mshtuko na majonzi baa da ya wanafunzi zaidi ya 40 wa Shule ya Sekondari ya Shauritanga waliokufa kwa ajali ya moto bwenini Juni 18, mwaka 1994.
Habari hii imeandikwa na Marc Nkwame na Veronica Mheta, Arusha.